13 Aug 2011

Adabu na tabia njema

Mwenyezi Mungu ametufunza adabu za namna nyingi ili ziwe pambo letu Waislam zikitupamba katika matendo yetu, maneno yetu, na pia zikitupamba ndani ya nafsi zetu.

Mapambo ya ndani ya nafsi ni Tabia njema. Na Adabu, ni yale maneno na matendo mema yanayozidhihirisha.


Neno Adabu, asili yake linatokana na neno ‘Maaduba’, na maana yake ni kualikwa chakula au kuitwa. Na neno ‘Adabu’, limetoholewa kutoka katika neno hilo ‘Maaduba’, kwa sababu watu ‘Wanaitwa’ katika kuzifuata tabia njema na katika kuwa na khuluka njema.

Khuluka njema ni msingi madhubuti wa Umma. Ni kuendelea kwa Umma. Ni tumaini la Umma. Ni uhai wa Umma.

Umma ukirudishwa nyuma kwa sababu zozote zile za kilimwengu kisha ukapoteza tabia zake njema na khuluqa zake, si rahisi tena kunyanyuka. Lakini Umma hata ukirudi nyuma namna gani, ikiwa bado umeshikamana na khuluqa njema, basi tumaini la kunyanyuka tena linabaki. Na hii ni kwa sababu Umma wowote ukiacha tabia zake njema na kujifanya kama karagosi kwa kuonyesha kila fani ya kuiga, na jeuri na utovu wa adabu, basi tamaa ya kunyanyuka tena inapotea.

Mshairi alisema:


“Hakika ya umma wowote ule ukitaka kubaki, basi lazima wawe na tabia njema. Tabia njema zao zikitoweka, basi na wao watatoweka.”


Umma wa Kiislamu ni Umma uliolelewa kwa Adabu na Tabia njema tokea Mtume wetu Muhammad (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alipoanza kuwalingania watu katika dini hii tukufu.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alikuwa akisema:

بُعِثْتُ لأتمِّمَ مَكَارِمَ الأَخْلاَقِ

“Kwa hakika nimeletwa kuja kukamilisha (kufundisha) tabia njema”.


Huyu ni Mtume wetu mtukufu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ambaye Mola wake alimsifia na kumwambia:

وإنك لعلى خلق عظيم

“Na bila shaka una tabia njema kabisa”

Al Qalam – 4


Muislamu anatakiwa awe mwenye adabu na mwenye heshima akiwaheshimu wakubwa wake na wadodo wake.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

<ليس منا من لم يرحم صغيرنا، ويعرف شرف كبيرنا>

Hayupo pamoja nasi asiyewahurumia wadogo wetu na asiyeijuwa heshima ya wakubwa wetu.

Attirmidhy na Abu Daud


Na katika riwaya nyingine, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema kumuambia Ummu Salamah (Radhiya Llahu anha):

يا أم سلمة ذهب حسن الخلق بخير الدنيا والآخرة

Ewe Ummu Salamah, Tabia njema imechukuwa kheri zote za dunia na akhera.

Attabarani


Muislamu asiyekuwa na adabu anaudhuru Uislamu badala ya kuupa nguvu. Mamilioni ya watu waliingia katika dini hii tukufu kwa kuvutiwa na Adabu na Tabia njema za Masahaba (Radhiya Llahu anhum) waliozifungua nchi zao hizo, pamoja na kuvutiwa na Adabu na Tabia njema za wale waliokuja baada yao.

Mataifa makubwa kama vile Indonesia kwa mfano, mamilioni ya watu wake waliingia katika dini hii kutokana na tabia njema za wafanya biashara wa Kiislam waliokwenda huko. Walikuwa wakiuona uaminifu wao, ukweli wao, ucha Mungu wao. Ilikuwa mara tu unapofika wakati wa Swala, walikuwa wakiwaona namna gani wafanya biashara hao wakiacha kazi zao na kuelekea mwahali maalum kwa ajili ya kufanya Ibada zao.

Imam Malik anasema:

“Umma huu hauwezi kutengenea isipokuwa kwa kufuata mwenendo wa wenzao waliowatangulia”.


  • Kuwatii wazee wawili
Kuwatii wazee wawili ni miongoni mwa Adabu zilizotiliwa mkazo sana na kusisitizwa katika Qurani na katika mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam).

Mwenyezi Mungu ametuamrisha tuwatii na kuwafanyia wema wazee wetu, na akazifanya haki za wazee - baba na mama - kuwa katika daraja la pili baada ya haki Zake Subhaanahu wa Taala. Mwenyezi Mungu amewajaalia wazee kuwa ni sababu ya kuwepo kwetu hapa duniani, na kwa ajili hiyo wakapata tabu sana juu yetu.

Hasa Mama, aliyembeba mwanawe tumboni miezi tisa, akamzaa, kisha akahangaika naye na kutaabika naye, tabu juu ya tabu. Tabu ya kubeba, tabu ya kuzaa, tabu ya kulea, kunyonyesha pamoja na kukesha na kuhangaika naye kila mtoto anapolia au kuugua.

Kwa ajili hiyo Mwenyezi Mungu Ametuamrisha kuwakirimu wazee wetu wawili hao, kuwatumikia kuwainamishia bawa la unyenyekevu, pamoja na kuwaombea dua ili Mwenyezi Mungu awarehemu kama walivyotulea huku wakiturehemu tulipokuwa watoto.

Mwenyezi Mungu Anasema:

وَقَضَى رَبُّكَ أَلاَّ تَعْبُدُواْ إِلاَّ إِيَّاهُ وَبِالْوَالِدَيْنِ إِحْسَانًا إِمَّا يَبْلُغَنَّ عِندَكَ الْكِبَرَ أَحَدُهُمَا أَوْ كِلاَهُمَا فَلاَ تَقُل لَّهُمَآ أُفٍّ وَلاَ تَنْهَرْهُمَا وَقُل لَّهُمَا قَوْلاً كَرِيمًا 23 وَاخْفِضْ لَهُمَا جَنَاحَ الذُّلِّ مِنَ الرَّحْمَةِ وَقُل رَّبِّ ارْحَمْهُمَا كَمَا رَبَّيَانِي صَغِيرًا 24


“Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa; Msimuabudu yeyote ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye yuko kwako, au wote wawili, basi usimwambie hata: Ah! Wala usiwakemee. Na sema nao kwa msemo wa hishima.

Na uwainamishie bawa la unyenyekevu kwa kuwaonea huruma. Na useme: Mola wanguMlezi! Warehemu kama walivyo nilea utotoni.”

Al israa- Bani Israil 23-24


Na Anasema:

وَوَصَّيْنَا الْإِنسَانَ بِوَالِدَيْهِ حَمَلَتْهُ أُمُّهُ وَهْنًا عَلَى وَهْنٍ وَفِصَالُهُ فِي عَامَيْنِ أَنِ اشْكُرْ لِي وَلِوَالِدَيْكَ إِلَيَّ الْمَصِيرُ

“Na tumemuusia mtu kwa wazazi wake wawili. Mama yake ameichukua mimba yake kwa udhaifu juu ya udhaifu, na kumwachisha ziwa baada ya miaka miwili. (Tumemuusia):Nishukuru Mimi na wazazi wako. Na kwangu Mimi ndiyo marudio.”

Luqman 14


Mafundisho ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) yanakubaliana na mafundisho ya Qurani.

Alipoulizwa juu ya matendo anayoyapenda zaidi Mwenyezi Mungu kupita yote, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alisema:

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) alisema:

"الصلاة على وقتها ثم بر الوالدين ثم الجهاد في سبيل اللّه"

"Swala ndani ya wakati wake, kisha kuwafanyia wema wazee wawili kisha jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu."

Fathi l Bari (Sharhi ya Sahihul Bukhari)


Aliiweka amali hii ya kuwafanyia wema wazee wawili kuwa ni ya pili ikiitangulia hata Jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu.


Na alipokuwa akizitaja amali ovu, akaitaja amali ya kuwaasi wazee wawili kuwa ni ya pili baada kumshirikisha Mwenyezi Mungu. Akasema:

قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: (ألا أنبئكم بأكبر الكبائر). قلنا: بلى يا رسول الله، قال: (الإشراك بالله، وعقوق الوالدين - وكان متكئاً فجلس فقال - ألا وقول الزور، وشهادة الزور، ألا وقول الزور، وشهادة الزور). فما زال يقولها، حتى قلت: لا يسكت.

Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam):

“Nikuambieni ni amali zipi zilizo ovu kupita zote?”

Tukasema:

“Tuambie ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu”

Akasema:

“Kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kuwaasi wazee wawili,”

Alikuwa ameegemea, akakaa vizuri, kisha akasema:

“Na kusema uongo, na kutoa ushahidi wa uongo…”

Akawa anayakariri maneno hayo mpaka tukasema (nyoyoni);

“Yareti angenyamaza”

Bukhari na Muslim


Pakitokea mgongano baina ya haki ya Mwenyezi Mungu na haki ya wazee, kwa mfano mzee awe ni mshirikina akimuamrisha mwanawe naye awe kama yeye katika ushirikina huo, au katika kumuasi Mwenyezi Mungu kwa jambo lolote lile, basi hapo haijuzu kumtii mzee, kwa sababu haki ya Mwenyezi Mungu ni kubwa zaidi na tukufu zaidi. Lakini wakati huo huo kuasi au kumshirikisha Mwenyezi Mungu kwao, kusikuzuwie kuwatendea mema na kusikufanye ukawa unawapiga pande.

Mwenyezi Mungu anasema:

وَإِن جَاهَدَاكَ عَلى أَن تُشْرِكَ بِي مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ فَلَا تُطِعْهُمَا وَصَاحِبْهُمَا فِي الدُّنْيَا مَعْرُوفًا وَاتَّبِعْ سَبِيلَ مَنْ أَنَابَ إِلَيَّ ثُمَّ إِلَيَّ مَرْجِعُكُمْ فَأُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ

“Na pindi wakikushikilia kunishirikisha na ambayo huna ilimu nayo, basi usiwat'ii. Lakini kaa nao kwa wema duniani, nawe ishike njia ya anayeelekea kwangu. Kisha marejeo yenu ni kwangu Mimi, na Mimi nitakuambieni mliyokuwa mkiyatenda.”

Luqman -15


Ndugu wa Nasaba ni wale ulohusiana nao, jamaa zako, ikiwa ni katika wanaoweza kukurithi au wasioweza, unaoweza kuoana nao au usioweza, lakini upo uhusiano wa nasaba baina yenu.

Mwenyezi Mungu Ametutahadharisha juu ya hatari ya kuwapiga pande ndugu wa Nasaba Akasema:

أَيُّهَا النَّاسُ اتَّقُواْ رَبَّكُمُ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن نَّفْسٍ وَاحِدَةٍ وَخَلَقَ مِنْهَا زَوْجَهَا وَبَثَّ مِنْهُمَا رِجَالاً كَثِيرًا وَنِسَاء وَاتَّقُواْ اللّهَ الَّذِي تَسَاءلُونَ بِهِ وَالأَرْحَامَ إِنَّ اللّهَ كَانَ عَلَيْكُمْ رَقِيبًا

“Enyi watu! Mcheni Mola wenu Mlezi aliyekuumbeni kutokana na nafsi moja, na akamuumba mkewe kutoka nafsi ile ile. Na akaeneza kutokana na wawili hao wanaume na wanawake wengi. Na tahadharini na Mwenyezi Mungu ambaye kwaye mnaombana, na jamaa zenu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuwaangalieni.”

Annisaa - 1

Hapa Mwenyezi Mungu anatutahadharisha tusije tukamuasi, na pia anatutahadharisha juu ya Jamaa zetu, tusije tukawapiga pande na kuachana nao.

Mwenyezi Mungu pia ametutaka tushikamane na kuendeana nao.

Mwenyezi Mungu anasema:

وَإِذْ أَخَذْنَا مِيثَاقَ بَنِي إِسْرَائِيلَ لاَ تَعْبُدُونَ إِلاَّ اللّهَ وَبِالْوَالِدَيْنِ إِحْسَاناً وَذِي الْقُرْبَى وَالْيَتَامَى وَالْمَسَاكِينِ وَقُولُواْ لِلنَّاسِ حُسْناً وَأَقِيمُواْ الصَّلاَةَ وَآتُواْ الزَّكَاةَ ثُمَّ تَوَلَّيْتُمْ إِلاَّ قَلِيلاً مِّنكُمْ وَأَنتُم مِّعْرِضُونَ

“Na tulipofunga agano na Wana wa Israili: Hamtamuabudu yeyote ila Mwenyezi Mungu; na muwafanyie wema wazazi na jamaa na mayatima na masikini, na semeni na watu kwa wema,na shikeni Swala, na toeni Zaka. Kisha mkageuka isipo kuwa wachache tu katika nyinyi; na nyinyi (pia) mnapuuza.”

Al Baqarah - 83


Na Akasema:

وَأُوْلُواْ الأَرْحَامِ بَعْضُهُمْ أَوْلَى بِبَعْضٍ

“Na ndugu wa nasaba wanastahikiana wenyewe kwa wenyewe”

Al Anfal – 75

Na Akasema:

فَآتِ ذَا الْقُرْبَى حَقَّهُ وَالْمِسْكِينَ وَابْنَ السَّبِيلِ ذَلِكَ خَيْرٌ لِّلَّذِينَ يُرِيدُونَ وَجْهَ اللَّهِ وَأُوْلَئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ

“Basi mpe jamaa haki yake na masikini na msafiri (aliyeharibikiwa). Hayo ni bora kwa wale wanaotaka radhi ya Mwenyezi Mungu; na hao ndio watakaofuzu”.

Ar Rum – 38


(Neno ‘Rahim’ maana yake ni ‘undugu wa nasaba’)

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenyezi Mungu amelitoa (au amelitohoa) jina la ‘Rahim’ kutoka katika jina lake ‘Al Rahiym’, kisha akasema:

“Atakayekuunga nitamuunga na atakayekukata nitamkata”.

Na hii inamaanisha kuwa Mwenyezi Mungu atamkata (kwa kutomrehemu) yule atakayeukata uhusiano na jamaa zake, na atawaunga (kwa kuwarehemu) wale watakaouendeleza uhusiano huo.


Mtu anaweza kuona kuwa; katika kutembeleana kwa ajili ya kuunganisha uhusiano na ndugu wa nasaba pesa nyingi zinatumika na wakati mwingi unapotea. Lakini Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) ametufundisha kinyume na hivyo.

Katika hadithi ilisiyomuliwa na Anas bin Malik (Radhiya Llahu anhu), Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Anayependa atandaziwe riziki (aongezewe riziki yake), basi aendeleze uhusiano wake na ndugu zake wa nasaba (jamaa zake alohusiana nao)”.

Bukhari

Na katika Hadith al Qudusiy, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenyezi Mungu ameiambia Rahim; ‘Je utaridhika iwapo nitamuunga atakayekuunga na nitamkata atakayekukata?”

Rahim ikasema:

“Ndiyo”

Mwenyezi Mungu Akasema:

“Basi hiyo ni haki yako”

Bukhari


Kuuendeleza uhusiano huu kunakuwa kwa kupendana, kunasihiana, kufanyiana wema na uadilifu, kurudishiana haki zilizopotea, kuwasaidia wale wenye shida kati yao, kujua hali zao, kusameheana katika makosa yanayotokea baina yao mara kwa mara, kuombeana dua, na kwa ujumla kujaribu kuwafanyia kila la kheri na kuwaepusha na kila shari kwa uwezo wote.

Iwapo katika ndugu, yupo au wapo wasiopenda kurudisha uhusiano na ndugu kwa sababu ndugu yake au jamaa yake huyo anapindukia mipaka katika kumuasi Mwenyezi Mungu, na baada ya kujaribu kila njia katika kunasihi kwa kutumia njia mbali mbali za hekima kujaribu kumweka sawa ndugu huyo bila mafanikio, basi hapana ubaya kuepukana na mtu au watu wa aina hiyo, wakati huo huo tukiendelea kuwaombea dua, huenda Mwenyezi Mungu akawahidi na kuwaongoza katika haki.


Mwenyezi Mungu anasema:

وَاعْبُدُواْ اللّهَ وَلاَ تُشْرِكُواْ بِهِ شَيْئًا وَبِالْوَالِدَيْنِ إِحْسَانًا وَبِذِي الْقُرْبَى وَالْيَتَامَى وَالْمَسَاكِينِ وَالْجَارِ ذِي الْقُرْبَى وَالْجَارِ الْجُنُبِ وَالصَّاحِبِ بِالجَنبِ وَابْنِ السَّبِيلِ وَمَا مَلَكَتْ أَيْمَانُكُمْ إِنَّ اللّهَ لاَ يُحِبُّ مَن كَانَ مُخْتَالاً فَخُورًا

“Muabuduni Mwenyezi Mungu wala msimshirikishe na chochote. Na wafanyieni wema wazazi wawili na jamaa na mayatima na masikini na jirani wa karibu na jirani wa mbali, na rafiki wa ubavuni na mpita njia, na walio milikiwa na mikono yenu ya kulia. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi wenye kiburi wanao jifakhiri”.

Annisaa – 36

Na katika hadithi iliyotolewa na Bukhari, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Jibril alikuwa akiendelea kuniusia juu ya Jirani, hata nilidhania atapewa haki ya kunirithi”

Kumfanyia wema jirani, ni kwa kutokumuudhi au kumkera.

Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Wallahi si Muislam Wallahi si Muislam”,

Wakamuuliza:

“Nani huyo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?”

Akasema:

“Ambaye jirani yake haiepuki shari yake”


Katika wema pia, ni kumfanyia jirani ihsani kiasi cha uwezo wako kwa kumsaidia pale anapohitajia msaada wao, kwa kumjulia hali yake, kumpelekea zawadi, yote hayo kiasi cha uwezo.


Mwenyezi Mungu anasema:


يَسْأَلُونَكَ مَاذَا يُنفِقُونَ قُلْ مَا أَنفَقْتُم مِّنْ خَيْرٍ فَلِلْوَالِدَيْنِ وَالأَقْرَبِينَ وَالْيَتَامَى وَالْمَسَاكِينِ وَابْنِ السَّبِيلِ وَمَا تَفْعَلُواْ مِنْ خَيْرٍ فَإِنَّ اللّهَ بِهِ عَلِيمٌ

“Wanakuuliza watoe nini? Sema: Kheri mnayo itoa ni kwa ajili ya wazazi na jamaa na mayatima na masikini na wasafiri. Na kheri yoyote mnayo ifanya Mwenyezi Mungu anaijua”.

Al Baqarah - 215


Na akasema:


وَإِذَا حَضَرَ الْقِسْمَةَ أُوْلُواْ الْقُرْبَى وَالْيَتَامَى وَالْمَسَاكِينُ فَارْزُقُوهُم مِّنْهُ وَقُولُواْ لَهُمْ قَوْلاً مَّعْرُوفًا

“Na wakati wa kugawanya wakihudhuria jamaa na mayatima na masikini, wapeni katika hayo mali ya urithi, na semeni nao maneno mema”.

An Nisaa - 8


Na akasema:

فَآتِ ذَا الْقُرْبَى حَقَّهُ وَالْمِسْكِينَ وَابْنَ السَّبِيلِ ذَلِكَ خَيْرٌ لِّلَّذِينَ يُرِيدُونَ وَجْهَ اللَّهِ وَأُوْلَئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ

“Basi mpe jamaa haki yake, na masikini, na msafiri. Hayo ni kheri kwa watakao radhi ya Mwenyezi Mungu. Na hao ndio wenye kufanikiwa”.

Ar Rum - 38

Na katika hadithi, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Mwenye kujishughulisha kuwasaidia Vizuka na Masikini ni mfano wa anayepigana Jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu, au mfano wa mwenye kufunga nyakati za mchana na kuswali nyakati za usiku”.

Bukhari

Na katika hadithi nyingine Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:

“Mimi na mwenye kumlea yatima tutakuwa (pamoja) Peponi kama hivi.” Akaashiria kwa kidole cha shahada na cha kati.

Bukhari

No comments:

Post a Comment